Thursday, November 01, 2007

Sakata la Wafanyakazi Bongo

Nilishasema. Serikali kuongeza mishahara kwa kiwango walichoongeza kitakosesha watu kazi. Na kweli hivi majuzi tulisikia makampuni kama Urafiki waliachisha wafanyakazi kwa wingi.

Nakumbuka ma baa medi walisherkea kusikia kuwa watalipwa shs.80,000/-. Lakini wangapi watabaki na kazi? Pia mahausigeli wanatakiwa walipwa 65,000/- kwa mwezi. Je mwajiri wake analipwa shs. ngapi?

Mishahara mipya ilikuwa ianze kulipwa leo lakini serikali wamesogeza hadi januari mwakani. Ila mshahara wa mahaugeli unaanza leo.

*******************************************************************************

From ippmedia.com

Waliofukuzwa kazi warejeshwe - Serikali

2007-11-01

Na Beatrice Bandawe, Dodoma

Serikali imewaagiza waajiri wote waliowafukuza kazi wafanyakazi wao kwa madai ya tangazo la mishahara mipya kuwarudisha kazini mara moja. Tamko la serikali lilitolewa na Waziri wa Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana, Bw. John Chiligati, wakati wa mkutano na waandishi wa habari uliofanyika mjini hapa.

Sambamba na hilo, serikali imetangaza kuwa viwango vipya vya mishahara vya sekta binafsi vitaanza kulipwa Januari Mosi, mwakani badala ya leo kama ilivyotangazwa awali na serikali. Waziri alisema kusogezwa mbele kwa muda wa kulipa mishahara hiyo kumetokana na maombi ya waajiri wa sekta yaliyowasilishwa serikalini wakiomba muda wa kujitayarisha kwanza.

Akizungumzia kusimamishwa ama kupunguzwa wafanyakazi alisema serikali imewaagiza waajiri hao kujipanga na bajeti yao mpya ili wawalipe wafanyakazi wao mishahara mipya ifikapo Januari mosi mwakani. Alisema mwajiri atakayeshindwa kumlipa mfanyakazi katika muda uliopangwa atachukuliwa hatua.

Aliwaonya baadhi ya waajiri wanaotaka kugeuza zoezi hilo kuwa la balaa badala ya neema. Aidha, Bw. Chiligati alisema kwa waajiri wa viwandani ambao walilalamika kuwa kupanda kwa mishahara hiyo kutaathiri mapato yao na kusababisha kupanda kwa bei za bidhaa, amewaagiza wakae na bodi zao kutoa mapendekezo na kuyawasilisha serikalini ili kuangalia athari zitakazojitokeza.

Waziri aliwaomba wafanyakazi kuwa wavumilivu wakati waajiri wanaandaa mishahara yao. Aidha, alisema kuanzia sasa waajiri wa sekta binafsi watatakiwa kuwaongeza wafanyakazi mishahara kila mwaka kama ilivyo kwa watumishi wa umma. Kutangazwa kwa viwango hivyo kunafuatia sekta binafsi kukaa muda mrefu bila kuwaongezea wafanyakazi mishahara yao.

Alisema wafanyakazi katika sekta hiyo tangu mwaka 2002 hawajaongezewa mishahara na kubaki na kima kile kile kwa kipindi cha miaka mitano. Bw. Chiligati alisema Oktoba mwaka huu serikali ilitangaza viwango vipya vya mishahara ya kima cha chini kwa sekta binafsi ambapo mishahara wa chini kabisa ni Sh. 65,000 kwa wafanyakazi wa ndani kilichotakiwa kutekelezwa kuanzia leo.

Hata hivyo, aliongeza kuwa baada ya kutangaza hatua hiyo, iliwastua waajiri wengi kwa kuwa hawakuwa wamejiandaa na wengine walianza kupunguza watumishi wao. Waziri alisema sekta ya viwanda, hasa ya nguo, ndiyo iliyopunguza wafanyakazi wengi na kuongeza kuwa waajiri wa sekta hiyo walipeleka malalamiko wizarani, wakisema tangazo hilo limekuja ghafla sana na kuomba wapewe muda wajitayarishe kwanza.

Alizungumzia wafanyakazi wa sekta ya kilimo, alisema kuna wale walio katika mashamba makubwa kama ya miwa, maua na tumbaku ambao walisema viwango vyao vya mishahara ya kima cha chini vimekuwa sawa na wale wanaofanya kazi kwenye mashamba madogo bila kuangalia uwezo. Alifafanua kuwa Bodi pia itakaa na sekta hiyo ili kuangalia mapendekezo yao. Bw. Chiligati alisema wafanyakazi wanaozalisha zaidi wana haki ya kulipwa vizuri ili waongeze tija kazini. Akitoa ufafanunuzi kuhusu mishahara ya wafanyakazi wa ndani, Bw. Chiligati, alisema kumekuwa na upotoshaji mkubwa kuhusu mishahara hiyo.

Alifafanua kuwa wafanyakazi wa ndani wanaofanya kwa mabalozi, mishahara yao ni Sh. 90,000, wakati wale wanaofanya kwa watumishi wa serikali wanatakiwa kulipwa Sh. 80,000 na wale walioko kwa watu wa kawaida watalipwa Sh. 65,000 lakini kama hawakai nyumbani kwa mwajiri. Alisema kwa wanaoishi nyumbani kwa mwajiri kati ya hizo Sh. 65,000, watakatwa asilimia 68 ya mshahara wake.

Kuhusu wafanyakazi hao kulipiwa michango ya Shirika la Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) na waajiri wao, Bw. Chiligati alisema serikali itakaa na Chama cha Wafanyakazi Mahotelini na Majumbani (CHODAWU), kujadili hilo.

Aidha, alisema sheria mpya ya kazi inakataza ajira za kienyeji na kuwataka waajiri kuhakikisha kunakuwepo na mikataba. Alitaja aina za mikataba hiyo kuwa ni ile ya muda, ya kudumu na ya kulipana kila siku.
SOURCE: Nipashe

1 comment:

Anonymous said...

Serikali watamzame upya hizo nyongezo. la sivyo wizi na ujambazi utazidi Bongo.